Ismail Haniyah pia amelaani mkutano wa hivi punde kati ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony Blinken na watawala wa Israel, wakati Israel ikiwa inashadidisha mashambulizi yake ya mabomu katika ardhi ya Palestina, ambapo inalenga hospitali, magari ya kubebea wagonjwa na raia wanaokimbilia usalama. Amesema kuwa Ikulu ya Marekani imetoa idhini kwa Utawala wa Kizayuni kuendelea na ukatili wake.
"Mauaji ya umati yanayofanywa na utawala wa Kizayuni ni dhihirisho la wazi la kinamasi ambacho utawala utawala ghasibu wa Israel umetumbukia katika Ukanda wa Ghaza," kiongozi huyo wa Hamas alisema.
Haniyah pia alitoa wito kwa mataifa ya Kiarabu na Kiislamu pamoja na watu wanaopenda uhuru duniani kueleza kwa sauti ghadhabu yao juu ya mauaji makubwa ya Wapalestina mikononi mwa majeshi ya Israel.
Aliziomba mamlaka za Misri kufungua tena kikamilifu kivuko cha mpaka cha Rafah kwa mujibu wa wajibu wao kwa wakazi wa Ukanda wa Gaza, ili misaada yote ya kibinadamu na bidhaa za kimsingi ziweze kuingia katika eneo hilo.
Amesema harakati za muqawama na mapambano zitaendelea kwa nguvu kulinda taifa la Palestina. Aidha amesisitiza kuwa maghasibu Waisraeli hawatapata nafasi katika ardhi ya Palestina.
Mkuu wa Ofisi ya Kisiasa ya Hamas pia amesisitiza ulazima wa kusitishwa kikamilifu mashambulizi ya Israel na mauaji ya halaiki ya Wapalestina huko Ghaza, na ameitaka jumuiya ya kimataifa itekeleze majukumu yake ya kibinadamu, kimaadili na kisiasa katika kukomesha jinai za kivita za utawala wa Kizayuni.
4179919