Sheikh Ahmad Tayyib, Sheikhe Mkuu wa Kituo cha Al Azhar cha Misri ametuma ujumbe akiwahutubu viongozi wa nchi mbalimbali duniani kwamba: "Mimi nikiwa Muislamu ambaye moyo wangu unaumia kutokana na mateso na masaibu ya raia madhulumu wa Palestina na mauaji ya wanawake na watoto wasio na ulinzi katika ardhi hiyo, nasema, wakati umefika kwa vita na jinai za utawala ghasibu wa Israel kukomeshwa katika ardhi za Palestina."
Sheikh Ahmad Tayyib ameongeza kuwa: 'Vita hivi vikiendelea, hakutakuwa na taifa kwa ajili ya watoto na vizazi vijavyo.' Sheikhe Mkuu wa Kituo cha Al Azhar pia aliwahi kuandika barua akiwahutubu viongozi wa Kiarabu ambapo alisema juhudi za kukomesha uvamizi wa adui dhidi ya ndugu zetu huko Palestina ni wadhifa wetu wa kidini na jukumu letu mbele ya Mwenyezi Mungu.
Katika barua yake hiyo kwa viongozi wa Kiarabu, Sheikh Ahmad Tayyib alisema: 'Sote tunataraji kuwa kwa kustafidi na uwezo wetu wote tutaweza kuzishinda dhulma na ukandamizaji wa utawala wa Kizayuni.'
Jeshi la utawala wa Kizayuni linaendeleza pakubwa mashambulizi ya anga, nchi kavu na baharini dhidi ya maeneo mbalimbali ya Ukanda wa Gaza ambayo yamegeuka na kuwa uharibifu mtupu. Mashambulizi hayo yameingia katika siku ya 59 tangu utawala wa Kizayuni uanzishe vita dhidi ya Gaza; kwa kadiri kwamba Wazayuni maghasibu mbali na kuyashambulia makazi ya raia na skuli moja ya chekechea katika ukanda huo, unashambulia pia magari ya misaada ya huduma za uokoaji.
Tume huru ya haki za binadamu huko Palestina imeeleza kuwa asilimia 80 ya wakazi wa Ukanda wa Gaza wamelazimika kuhama makazi yao kutokana na hali mbaya ya kibinadamu katika maeneo hayo.
4185619