Wilders mwenye siasa kali za mrengo wa kulia wa Uholanzi , ambaye chama chake kilishinda uchaguzi wa hivi karibuni nchini humo, alitoa makubaliano muhimu kwa vyama ambavyo vinaweza kuwa washirika wa muungano siku ya Jumatatu, na kutangaza kwamba anaondoa sheria ambayo alipendekeza mnamo 2018 inayotaka kupigwa marufuku kwa misikiti na Qur'ani Tukufu.
Hatua hiyo imekuja siku moja kabla ya mazungumzo ya kuunda serikali ijayo kupangwa kuanza tena, kufuatia uchaguzi wa Novemba.
Kuacha pendekezo hilo kunaweza kuwa muhimu katika kupata uungaji mkono na vyama vingine vitatu vikuu ambavyo Wilders anataka kuvijumuisha katika muungano pamoja na Chama chake kinachojulikana kwa kifupi kama PVV.
Mmoja wa viongozi wa vyama hivyo, Pieter Omtzigt wa Mkataba Mpya wa Kijamii wa mageuzi, ameelezea hofu kwamba baadhi ya sera za Wilders zinakiuka Katiba ya Uholanzi ambayo inasisitiza uhuru, ikiwa ni pamoja na uhuru wa dini.
Wakati wa mjadala wa bunge mwaka jana baada ya chama cha PVV kushinda viti 37 katika bunge la Uholanzi lenye viti 150 katika uchaguzi mkuu wa Novemba 22, Wilders aliashiria kulegeza msimamo wa chama chake dhidi ya Uislamu.
3486738